Utangulizi
Kati ya  dhambi ambazo kwa wakatoliki ndiyo wazi kwa watu ni dhambi ya kuabudu sanamu. Dhambi hii imewafanya wakatoliki waonekane au hawasomi Biblia au wanasoma ila hawaelewi au wanasoma na kuelewa lakini wamekuwa wakipuuza maandiko Matakatifu. Ubayana wa dhambi hii kwa wakatoliki ni kile wanachokifanya siku ya Ijumaa Kuu na mambo yanayoonekana katika nyumba za kuabudia kama makanisa ambapo sanamu lukuki zinaonekana, toka zile za vitu vya duniani hadi vile za mbinguni.

Tuhuma kwa wakatoliki haitoki hewani, bali ni kutokana na mambo hayo kwenda kinyume na baadhi ya aya katika maandiko matakatifu. Law. 19:4; 1Yoh. 5:21; Zab.115:1 – 9)
Kifupi ni wazi kabisa kuwa kuziabudu sanamu ni kosa; na hata katika baadhi ya nukuu kuzichonga pia imeoneshwa kuwa ni kosa. (Kumb. 20:3 – 5 na Kumb. 5:7 – 10). Sisi wakatoliki tonazo sehemu nyingi tu tulikoweka hizo sanamu ndiyo maana tunatuhumiwa kuwa kinyume cha Maandiko Matakatifu.

Kwa nini wakatoliki wamechonga sanamu ingawa  imekatazwa (Kumb. 20:3 – 5 na Kumb. 5:7 – 10)?
Wakatoliki wameangalia roho ya katazo la kuchonga sanamu na si katazo lenyewe tu. Roho ya katazo la kutochonga sanamu haikuwa Mungu kuamua kuzichukia tu sanamu, la hasha! Bali Mungu aliwakataza waisrael wasichonge sanamu za vitu wala vya duniani wala vya mbinguni kwa sababu alijua kuwa waisrael ambao wakati ule walizungukwa na makabila ya kipagani ambayo yalikuwa na kawaida ya kuabudu sanamu. Ili kuwaepusha Waisraeli, ambao imani yao kwa Mungu mmoja  ilikuwa bado kukomaa, aliwakataza wasichonge. Kwa hiyo roho ya katazo hilo lilikuwa ni  hatari ya kuanza kuziabudu – kama walivyokuwa wanafanya wenzao wapagani.

Tunasema hivyo kwa sababu Mungu huyo huyo aliyewakataza Waisraeli kuchonga sanamu katika Kumb. 20:3 – 5, mbele kidogo anamwagiza Musa huyo huyo kuchonga sanamu ya makerubi katika sanduku la Agano (makerubi ni vitu vya mbinguni) ( Kumb. 25:18 – 20, Ebr. 9:5). Hapa Mungu ameonekana kutengua kile ambacho alisema pale mwanzoni kuwa wasichonge sanamu yoyote. Utenguzi huo si wakimaana; si wa kiroho ya sheria, bali ni wa kidhana ya katazo. Maana yake, Mungu anamruhusu Musa kuchonga sasa sanamu akijua kwamba Waisrael sasa wamekomaa kiimani kiasi kwamba hata wakichonga sanamu hawataweza kuiabuni ikichukua nafasi ya Mungu. Kwa hiyo roho ya katazo ilikuwa ni kutoabudu sanamu.

Kama haitoshi, ukienda mbele kidogo ya kitabu hicho cha Kumbukumbu la Torati Mungua anafanya mchezo wa hatari zaidi wa kumwambia Musa achonge nyoka wa shaba (kitu cha duniani) na kumweka kwenye mti na kila amtazamaye angepona. (Hes. 21: 8-9, Yoh. 3:14 – 15). Musa alitekeleza agizo hilo naye Mungu alimuhesabu kama mtiifu kwake. Hata hapa pia Mungu ameona kuwa waisraeli sasa imani yao kwa Mungu mmoja ni thabiti kiasi kwamba hata kama wakiona sanamu wasingeweza kuziabudu wakamsahamu Mungu wao. Si kwamba Mungu ana chuki na  sanamu, hata kidogo. Kama Mungu angekuwa na chuki na sanamu tusingeweza kuziona nukuu zifuatazo: Kut.  29:37, 1Fal. 7:29, Hek. 16:7.
Kifupi, imani ya mwanadamu hukua kama vile akili ya mtu inavyokua kutoka utoto, ujana hadi utu uzima. Mwanzoni kabisa waisraeli walikuwa kama watoto kiimani. Kumbuka Abrahamu alitoka kwenye nchi ya kipagani baadaye taratibu Mungu anamtoa kutoka katika utamaduni huo wa kuabudu miungu hadi kwenye kumwabudu Mungu mmoja. Kilele cha kumwabudu Mungu mmoja kinafikia pale mlimani sinai wanapopewa sheria. Kukua taratibu huko kwa imani ya waisrael ndiyo sababu inayofanya kuwepo tofauti ya nukuu za Mungu kukataza au kuruhusu kutengeneza sanamu. Hii ni sawa na mtoto anayekatazwa kushika kisu na mama yake lakini anapofikia umri wa kupevuka anaruhusiwa kushika kisu. Sisi wakatoliki siyo watoto wadogo kiimani hata tuogope kuchonga sanamu tusijeziabudu. Tunazichonga tukijua kwamba hata siku moja hazitaweza kutudhuru kwa sisi kuanza kuziabudu. Wale wote wanaogopa kuzichonga sanamu, wajue kuwa wao ni wachanga kiimani.

Kama Mungu hakatazi kuchonga sanamu ila anakataza kuzifanyia ibada, je, sisi wakatoliki hatufanyi hivyo?
Kujibu swali hilo, ndiyo nitakuwa nimegusa kiini cha swali lako Sr. Gracia. Nakuomba fuatilia maelezo yangu, huu ulikuwa kama utangulizi tu.

KUABUDU MSALABA

Kama wakristo, hatuna budi kujisifu kwa vile tumekombolewa kwa njia ya msalaba ambapo Bwana wetu Yesu Kristo alitundikwa na akafa juu yake. Lengo la Yesu ni kutuletea wokovu. Mimi na wewe tulistahili kupata adhabu hii ambayo yeye ameipata badala yetu. Kwetu msalaba ni ukombozi, msalaba ni sehemu ya maisha yetu na msalaba ni haki yetu. Hivyo msalaba ni lazima uheshimiwe na si kuabudiwa. Anayepaswa kuabudiwa ni Mungu peke yake. Zipo heshima za viwango tofauti:
Mungu kwanza (latria) – tunamwabudu.
Bikira Maria (Hyperdulia)
Watakatifu wengine na vitu wanavyohusika navyo (dulia)
Picha na sanamu pia hupewa heshima isiyoizidi ile ya watakatifu na Bikira Maria.
Hayo ndiyo madaraja ya heshima ambayo tunazitoa, 2 hadi 4 ni heshima tu.

Mpendwa Sr.Gracia,sijafikia ufundi wa kufafanua yote unayopenda kuyajua ila nataka nijaribu kadiri nitakavyoweza japo kwa kifupi kiha upitie.Yaliyo ya kizushi yafumbie macho na usiniseme nikatengwa na Kanisa. Nianze kwa kueleza maana ya neno sanamu kisha nitaendelea:

Sanamu
Ni kitu kilichochongwa au kutengenezwa kikiwakilisha kitu halisi,mtu,mnyama,mchoro au chochote kile kilicho halisi.Kwa hiyo ili kukiita sanamu,hicho ambacho kimetengenezwa,lazima kikiwakilishe kitu halisi,ndiyo maana ukitembelea sehemu za makumbusho utakuta sanamu za maraisi,nenda Butiama utaikuta sanamu ya Baba wa Taifa letu au kule Zanzibar utakuta sanamu ya mzee Karume n.k.Pamoja na hayo,kitu sanamu,kinaweza kikachukua mtindo wa picha.Mtu aliye na photo albam zile zote zilizomo iwe ni sura za watu,wanyama,miti au vitabu ni sanamu za hao au hicho kilichowakilishwa kwa njia ya hizo picha.Mtu akiandika kitabu cha historia kwa mfano,alichoandika si historia yenyewe kwa kuwa historia huwezi ukaiandika bali ataandika kiwakilishi cha historia ambacho amekiweka katika maandishi.Maandishi hayo{zile herufi} ni sanamu. Kwa maneno mengine,ukiwa huko shuleni unafundisha,herufi zote zilizomo kichwani mwako,ukiziandika tu ubaoni tayari elewa kuwa unaandika sanamu na wote watakayoyasoma hayo maandishi,wanasoma sanamu.Kwa kifupi,sanamu ya kila kitu inaanzia kichwani au akilini mwa mtu,anapoichonga au kuiandika au kuichora basi anaiumba kadili aijuavyo.Kitu halisi kinakuwepo lakini mwandishi au mchongaji amekiwakilisha kwa mtindo wake.

KUABUDU
Hiki daima ni kitendo cha kumtukuza mtu, kitu au chochote ambacho si mungu [herufi ndogo} kama vile unavyomtukuza Mungu {herufi kubwa}mwenyewe.Lazima kila mmoja atambue kuwa anayestahili kutukuzwa ni Mungu tu kama tunavyosoma katika Biblia Takatifu rej.Mdo 17:28 KWA KUWA NDIYE ANATUWEZESHA KWENDA NA KUFANYA CHOCHOTE, au rej Kumb 4:15/28,15:42ff sehemu ambazo Mungu ametukataza kuabudu kitu kingine chochote tofauti na yeye.

Je, tunapotuhumiwa kuwa tunaabudu sanamu wanatusingizia?Sanamu hutusaidiaje?
Lengo la kutumia sanamu ni pamoja na kutukumbusha kitu kilichokuwepo kwani ukufuatilia maelezo yangu juu ya neno sanamu utagundua kuwa huwezi kuitengeneza ya mtu ambaye bado hujamwona.Kwa hiyo zinatumika kama nyenzo ya kutukumbusha yaliyotokea zamani za kale. Ndivyo kwa mfano matumizi ya picha yaliyopoUkienda Nairobi kwenye malezi na huko ukaamua kupiga picha ukiwa katika barabara nzuri utaitunza kama ukumbusho wako na hiyo itakufanya ulikumbuke kwa urahisi tukio hilo kuliko kama ukisimulia tu.
Kuhusu suala la kuabudu ili mtu aambiwe kuwa ameabudu lazima awe ametimiza mambo makuu  mawili yaani:
1.     Kuwa na nia kamili ya kuabudu ile sanamu ikichukua nafasi ya Mungu
2.     Kufanya ibaada ya dhati  ya kuiabudu hiyo/hizo sanamu.
Kuna mambo kama tisa hivi ambayo mmoja anaweza kuyafanya akiwa katika ibada ya sanamu. Mambo hayo yametajwa katika Biblia Takatifu.
1.     Utoe sadaka Hos 4:13
2.     Uitolee sanamu yako ubani 1 Fal 11:8
3.     Ufanye tambiko mbele ya sanamu yako Isa 57:6
4.     Uitolee zaka Hes 2:8
5.     Uweke sanamu yako juu ya meza au tuseme iwepo meza Isa 65:11
6.     Usujudie sanamu yako 1Fal 19:18
7.     Uiinulie mikono sanamu yako Isa 44:20
8.     Uichezee ngoma sanamu yako 1Fal 18:26
9.     Ulale kifudifudi na kuipigia makofi sanamu yako (1Fal. 18:26).

Nini wafanyacho wakatoliki?
Kwanza, wakatoliki hawaamini juu ya miungu mingi kama walivyofanya watu wa kale.Hakuna mkatoliki anayedai kuwa Maria na Watakatifu ni miungu wala hawasemi kuwa msalaba una nguvu kuliko Mungu.Haya ni mashtaka ya watu wasiojua nini wakatoliki wanakifanya.Wayahudi kwa asili waliabudu miungu mingi hadi pale Mungu alipojifunua kwao na kuwataka waache kuiabudu miungu isiyo ya kweli.Pamoja na hayo katika safari yao ya maisha hawakuonesha kutii agizo la Mungu na matokeo yake waliweza kuiabudu hata miungu ya uongo.

Pili, Wakatoliki wanatambua kuwa Mungu ajua yote na hafungwi na muda.Kwa hekima kubwa aliyonayo,hawezi kuikasirikia sanamu ambayo inaheshimiwa tu kama ukumbusho wala haichukui nafasi yake.Mungu alikuwa akiwaadhibu vikali Wayahudi kwa kuwa kila walipohisi kuwa amewaacha,waliacha kumwamini wala kumwabudu yeye bali wakajitengenezea sanamu za kuchonga na hizo wakasemezana na kukubaliana kuwa ndo Mungu mwenyewe.Mungu alichukia na kuwaadhibu kwa vile waliziabudu na zikachukua hadhi kama ya Mungu wa kweli.


Tatu, Mungu kwa kutambua kuwa si kila sanamu imetengenezwa ili ichukue nafasi yake,aliweza kumruhusu hata Musa kutengeneza  sanamu kwa lengo maalumSehemu ambazo Mungu karuhusu sanamu ni nyingi sana katika Biblia rej. Hes 21:8f,Ebr 9:5, Yn 3:14f,Kut 16:31,2 Nyak 3:10, 4:4, Eze 41: 17 ff,n.k Kwanini anaruhusu?Kwa kuwa hazina madhara,zimetengenezwa kwa lengo lisilo la kuziabudu.


Je, tuseme nini juu ya kile tufanyacho Ijumaa Kuu?
Kitu cha msingi ni kusikiliza maneno ya Padre au shemasi anapowaalika watu kuja kuanza kuabudu.Padre au shemasi husema,
                     “Huu ndio mti wa msalaba, ambao wokovu wa dunia
                              umetundikwa juu yake, njooni tuuabudu”.
Ukifuatilia kwa makini kiswahili sanifu na bahati njema wewe mwalimu japo sijui wa somo lipi, utagundua kuwa, Padre hufanya mambo haya yafuatayo katika mwaliko huo:
1.     Hutuonesha mti wa msalaba.
2.     Hutuambia kuwa juu ya mti huo,wokovu umetundikwa
3.     Kisha hutualika tukauabudu.

Ningekuwa naongea nawe,ningekuuliza hivi hutualika tukauabudu mti wa msalaba au wokovu ambao umetundikwa juu ya huo mti au tukauabudu mti na msalaba au tukauabudu nini? Hebu fikiri kisha uone kama mawazo yako ni sawa na nitakachokisema hapa chini kabla hujaangalizia!

Wakatoliki hualikwa kufanya nini?
Kwa mwaliko huo,wakatoliki hualikwa kwenda kuuabudu WOKOVU ulio juu ya msalaba.WOKOVU NI NINI? WOKOVU  ni jina lililoandikwa kwa kiswahili.Jina wokovu kibiblia na kwa lugha asili ya Biblia ni sawa na jina YESHUA kwa kiebrania au YOSHUA. Mwanangu,wewe unamfahamu Yoshua katika Biblia kuwa alichukua jukumu la kuwaingiza Waisrael katika nchi ya ahadi baada ya Musa kufa kwani huyu ndiye aliyekuwa msaidizi wa Musa.Yoshua aliwachukua watu hawa wakiwa ng`ambo ya mto Yordan wakisubilia tu kuiingia nchi ya ahadi.Kumbe kwa Waisrael Yoshua ni mtu wa muhimu sana kwao kwani baada ya Musa kuwatoka,wanamtumainia Yoshua na kumwona kuwa ni Mwokozi wao kwa kitendo cha kuwafikisha salama katika nchi ya ahadi ambayo kwa miaka karibu 40 wamesafiri kuifikia.Tendo la Yoshua la kuyapiga maji ya mto yakagawanyika na kuacha nchi kavu nao wakavuka bila shida,ndilo wanaloliona kuwa la kuwaletea ukombozi kama alivyofanya Musa pale alipoyapiga maji ya bahari ya Sham yakaacha njia wakapita kwa usalama kutoka Misri.

Kristo ndiyo WOKOVU wetu tunayepaswa kumwabudu kwani alipokuja aliamua kuanzia kazi yake ya kutuletea wokovu katika mto Yordan pale ambapo Yoshua kahitimishia kazi yake.Yoshua aliwavusha watu toka ng`ambo ya mto kuwaingiza katika nchi ya ahadi ambayo ni Kanaan ya duniani na Yesu anapokuja,kama mwokozi,anataka awatoe watu wake kutoka katika nchi ya ahadi ya kidunia,kuwapeleka katika nchi ya ahadi ya mbinguni.Kumbe Yesu ni mwokozi wetu anayetutoa kutoka katika dunia kwenda mbinguni wakati Yoshua anaitwa mwokozi kwa kuwa aliwatoa Misri akawaleta Kanaan nchi ya ahadi.Yesu na Yoshua kwa mantiki hii ni hilo jina WOKOVU kama nomino wakati kazi waliyotenda ni ya kutuokoa na kikitamkwa kama kitendo,Yesu au Yoshua,anaitwa Mwokozi.

Labda nikupeleke kidogo darasani juu ya mambo ya viambishi katika lugha ya kiswahili kwani hapa ndipo wengi wanaposhindwa kueleza kile tunachokiabudu ile Ijumaa Kuu.
Padre au Shemasi husema ,
Huu ndiyo MTI wa msalaba ambao WOKOVU wa dunia Umetundikwa juu yake, njooni tuUabudu.
Katika sarufi ya kiswali hasa tunaposema juu ya upatanisho wa kisarufi, bahati mbaya ni kwamba nomino MTI na nomino WOKOVU zote zimechukua viambishi ngeli U, ili kuwa na upatanisho wa kisarufi. Tunasema kwa mfano, mti umaanguka, wokovu umetujia. Katika sentensi  hiyo anayotamka padre au shemasi, ina maneno yote mawili, yaani mti na wokovu yenye kiambishi kimoja tu U kinachotuletea shida kuwa kimaresha nini, wokovu au mti. Kiambishi U, hakirejerei mti bali kinarejea wokovu yaani Yesu.
Kwa hiyo tunaposema njooni tuuabudu, hatumaanishi tuuabudu mti la hasha! Bali tuuabudu Wokovu uliotundikwa juu ya mti wa msalaba katika akili zetu. Ndiyo kusema, ibada hii kama mtu hawezi kutoka nje ya pale na kupeleka mawazo yake kwa  Yesu, aliye Wokovu wetu , bila shaka anaweza kuwa anaabudu sanamu au mti wa msalaba.

Mpendwa sista, Kristo Bwana wetu ndiye sanamu ya kwanza kabisa ya Mungu. Ndiyo maana Kristo anasema aliyemwona Yesu kamwona Baba Yn 14:8f. Kama Yesu ni sanamu,hata binadamu ni sanamu za Mungu kwa vile tumeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.Kama mtu anaziogopa sanamu,ashakumu si matusi,aogope hata kuzaa watoto kwa vile kuzaa mtoto ni kuongeza sanamu duniani kwa kuwa licha ya kufanana na Mungu,zinafanana na mzazi mwenyewe.Kama hatuziabudu,yanini kuziogopa? Kama maandishi ni sanamu lakini hatuyaabudu,kwa nini uogope kusoma herufi? Mungu si mjinga wa kutuhukumu kwa mambo kama hayo yasiyochukua sifa yake.

Pamoja na hayo,tukumbuke kuwa sanamu huanzia kichwani mwa mtu kama nilivyokwishasema.Kama mtu akibuni kichwani kutengeneza gari nzuri sana,hatuwezi kumzuia kwa sababu atakapotengeneza kile alichonacho kichwani kikawa gari,hatakiabudu.La sivyo,hata kupanda gari ili kusafiri tuache kwani tunapanda
Ndani ya sanamu walizotengeneza watu.Ukiwa na picha zako,kwa jinsi zilivyotoka vizuri,ukafurahi na kuzibusu,haina maana kuwa unaziabudu.Au,kwa vile sasa unajua kuwa mtu ni sanamu ya Mungu,je ukienda mahali ukamsalimu mkubwa wako au anayekulea wakati unampa kitu ukampatia huku ukipiga goti, utakuwa unamwabudu?

Hatimaye, Kanisa katika sheria yake no.1159 linafundisha kuwa,sanamu ya Mungu haipo kwani tangu mwanzo Mungu baba hajawahi kuonwa na mtu isipokuwa kupitia kwa mwanae ambaye watu walimwona na waliishi naye wakamfahamu na kumbe kuchonga sanamu ya kufanana naye Isingeliwezekana.Sanamu za Yesu zafanana naye kwa vile watu walimfahamu alivyofanana lakini zimeletwa kwetu kama ukumbusho wa jinsi alivyokuwa si kwa lengo la kuziabudu. Kwa kuziona,hatuna mashaka kuwa alikuwepo kuliko kama tungekuta masimlizi tu.Hivyo hivyo kizazi kijacho kikiambiwa juu ya Nyerere kitaelewa zaidi kikioneshwa picha na sanamu zake lakini hizo picha na sanamu zake hawatasema ndo Nyerere mwenyewe labda kama ni vichaa.

HITIMISHO.
Mungu si mjinga wa kukasirikia kitu kisicho na madhara. Aliwaadhibu wote waliochonga sanamu na kusema hizo zafanana na Mungu lakini sisi hatusemi zinafanana naye bali tunajua kuwa yeye yupo na hizo zipo kama ukumbusho wa sura ya Yesu mwanae ambaye tunamfahamu kupitia waliomwona wakazitengeza. Akili zetu zinapata kutufanya tumtambue Kristo tunapoziona sanamu lakini kwa zenyewe si Kristo wala Mungu wetu
Ukiona sanamu ya B.Maria au Mtakatifu Fulani, ni uthibitisho kuwa, wapo watu waliomwona wakamchonga alivyo na sanamu yake inatukumbusha alivyokuwa nasi tunahizwa kuishi kwa mfano wake. Hakuna aliyewahi kumwona Mungu Baba hivyo hakuna awezaye kuchonga sanamu ya kufanana na Mungu, atachemka tu. Ndiyo maana waisraeli waliadhibiwa, walikuwa wanachonga ndama wanajidai eti Mungu anafanana na Ndama,hayuko hivyo wala hakuna aliyekwisha kumwona ni kutwanga maji kwenye kinu.Mwishowe umeanza kusinzia,naishia hapo pole kwa kukuchosha.

Kifupi, hapo mwanzo Mungu aliwakataza waisraeli kuchonga sanamu kwa sababu aliona imani yao kuwa ni changa wangeweza kuanza kuziabudu, baadaye aliwaruhusu akijua kuwa walikuwa wamekua kiimani kwake, hata wangechonga wasingeweza kuziabudu. Sisi tunachonga kwa sababu imani yetu kwa Mungu imekomaa na hivyo sanamu haziwezi kutufanya sisi tuanze kuziabudu. Juu ya siku ya Ijumaa kuu kinachoabudiwa ni WOKOVU ambao ni Yesu mwenyewe aliye Mungu na hivyo anapaswa kuabudiwa. Hatuabudu mti wa msalaba kwani ni kinyume na Maandiko Matakatifu na kinyume na amri ya kwanza ya Mungu.

Post a Comment

 
Top