KIFO NI HAKIKA

Jana nilikuwa kwenye Mazishi ya sista Dorothea Mkapuchini huko MAUA MOSHI. Jana hiyo hiyo amefariki ndugu  CHARLES CHISHIMBA Mkapuchini wa Custos ya Zambia.
Katika nasaha alizotoa mkuu wa Shirika Nd. Wolfgang Pisa OFMCAP ni tujenge utamaduni wa kukitafakari kifo. Mimi niliguswa sana na ujumbe wake na hapa nimeonelea niwashirikishe ijapokuwa si wengi mtaipenda hii Tafakari.


KIFO  NI HAKIKA
Kwa maana u mavumbi wewe nawe mavumbini utarudi (Mwa 3:19)
Kila Jumatano ya Majivu Kanisa hutukumbusha ukweli kwamba sisi ni mavumbi na mavumbini tutarudi. Siku inakuja ambapo mimi na wewe hakika tutakufa. Hali hii inamsubiri kila mmoja wetu awe tajiri au masikini, msomi au mjinga, mkleri au mlei, walio na nguvu au walio dhaifu, walio wema na walio waovu. Ni wakati wa kifo, wakati ambapo roho itauacha mwili, inaingia katika umilele, wakati mwili unarudia mavumbini.
Kifo kinaweza kukutenda nini? Wakati wa maisha inawezekana uliheshimika, ulifikiriwa, uliheshimiwa na kujienzi. Baada ya kifo mwili wako unakuwa ni kitu ambacho ni lazima tuachane nacho mara kwani uozo wake ni karaha kubwa. Ni lazima uzikwe haraka ukaingie katika zama za wafu.
Wakati wa maisha inawezekana ulijulikana sana, watu wakikuheshimu kutokana na busara zako, hekima, akili, uwepo wako na ulihitajika sana.
Baada ya kifo haitachukua muda utasahaulika mara. Watu watakaposikia juu ya kifo chako wengine wanaweza kusema: “Alikuwa mwema kwa familia yake, kwa shirika lake.”
·  Wengine watasikitika kwa sababu uwepo wako uliwafaidia –ndiye ulikuwa unawapatia mkate wa kila siku.
·   Wapo wanaofurahia kifo chako kwa kuwa kwa uwepo wako ulikuwa unawawekea kiwingu.
Wakiamini kwamba kwa kutokuwepo kwako ni kwa faida yao sasa. Lakini haitachukua muda kabla ya kusahaulika na hakuna atakayeongea juu yako.
Kwa siku chache baada ya kifo chako, ndugu zako na marafiki wako wa karibu watatetemeka watakaposikia jina lako wakiogopa kuibua tena hisia za huzuni. Lakini haitachukua muda watafarijiwa, pengine hata kwa wazo la kushiriki katika hali yako.
Kwa hiyo hata kwa wakati mfupi kifo chako kinaweza kuwa sababu ya furaha, na katika nyumba yako, pengine katika chumba kile ambapo ulifia, na kuhukumiwa na Yesu Kristo, wengine watafurahi na kucheza, kula na kunywa, na kucheza kama ilivyokuwa kabla ya kifo chako. Na roho yako itakuwa wapi?
Ndiyo maana unapaswa kukumbuka haya maneno ya ajabu: “Kumbuka kwamba wewe ni mavumbi na mavumbini utarudi.” Mambo yana mwisho, na ikiwa katika kifo utaipoteza roho yako, utakuwa umepoteza kila kitu kwako.
Mt. Lawrence Justinian, anatukumbusha kuwa, unapaswa kujiona mwenyewe kama ambaye amekwisha kufa, kwa kuwa unafahamu kuwa hakika utakufa siku moja, na ni hivi punde. Aliongeza, na kama umekwisha kufa, ni kipi ambacho usingalitamani kukifanya? Wakati unaishi kumbuka kwamba siku moja utakuwa kati ya wafu kama mmoja wao.
Mt. Bonaventura anasema ili kuiongoza meli salama, nahodha ni lazima daima abaki katika usukani. Kwa namna hiyo hiyo ili kuishi maisha mazuri na yenye tija, ni lazima kujiona mwenyewe katika saa ya kufa.
Wakati St. Camillus de Lellis alipopita makaburini na kuona makaburi ya wale waliolala alijisemea mwenyewe: “Ikiwa watu hawa wangaliweza kuishi tena, wangefanya nini ili waingie mbinguni? Ungefanya nini, wewe ambaye bado unaishi na mwenye muda wa kujiandaa kwa siku ya kifo yaani kumpokea dada mauti?
Kumbuka mfano ambao Yesu aliutoa kuhusu mtini usiozaa na maneno aliyoyasema kwa mtunzaji wa mti ule: “Tazama miaka mitatu hii naja nikitafuta matunda juu ya mti huu, nisipate kitu, uukate, mbona hata nchi unaiharibu?” Lk 13:7
Umekuwa hapa duniani kwa zaidi ya miaka mitatu. Umezalisha matunda ya aina gani mpaka sasa? Mt. Bernad anasema Bwana hafurahii tu maua, ila pia matunda ambayo ni matokeo ya uwepo wa maua. Ndiyo kusema kwamba Mungu hafurahii tu shauku yetu na ahadi tunazomwekea, ila zaidi mno matendo mema ambayo tunayafanya tungali bado hai.
Jifunzeni kuutumia muda vizuri mngali hapa duniani. Msisubiri mpaka muambiwe hakuna muda tena, au muda wa kuondoka hapa duniani umekaribia. Jiwekeni tayari kufa hata sasa ikiwa ni mapenzi ya Mungu. Kesheni kila wakati kwa kuwa hamjui saa.



Mwili kaburini 
Ndugu yangu Mkristo, ili upate kutambua kile ulicho, nenda makaburini ukatafakari ju ya kifo. Zingatia ushauri wa Mt. Yohani Chrisostom: “Nenda kaburini, tafakari juu ya mavumbi, majivu, wadudu na taka zilizopo humo. Hebu fikiri juu ya mzoga unavyojeuka kuwa njano kisha kuwa mweusi.
Haichukui muda mwili wote utakuwa umejaa usaha mweupe, wenye kutoa harufu kali ambayo hakuna anayependa kuivuta, fikiri juu ya unene wa nyamba unavyosambaratika na kuacha mifupa, jinsi ambavyo mchwa na wadudu wengine watakavyokuwa wanasherehekea kitoweo hicho. Hebu fikiri juu ya panya wa kila aina ambavyo wanakimbilia chakula hiki, wengine wakiingia midomoni na wengine tumboni na kwingineko kadiri wanavyoweza.
Ni wakati ambapo kila kitu kinaanguka iwe nywele, mikono na mengine. Mbavu zinaanikwa hadharani, kisha miguu na mikono inachomoka kutoka kwenye mashiko yake. Mchwa kisha kula kila kitu, wanabaki kushangaa mifupa ambayo pengine hawawezi sasa kuila, ni wakati ambapo mifupa inaanza kutengana kule kushikana kwake, fuvu la kichwa linaachana na kiwiliwili. Ama kweli mwanadamu si kitu. Huo ndio mwili unaokufa.
Tazama mtu ni nina! Ni kama mavumbi membamba yawezayo kupeperushwa na upepo kidogo. Watazame watu maarufu, masharifu, waliotawala mijadala mikubwa na kuonekana wamestawi kimaisha. Wamebaki kuwa historia! Nao wamekufa wamelala makaburini. Makaburi ni makao yao milele!
Walijijengea majumba makubwa, makasri, mahekalu, wakawa na magari ya kifahari! Walivaa mavazi ya Hariri! Popote walipopita waliheshimika sana! Walisalimiwa na kusujudiwa na watu! Leo hii wako wapi? Ukitaka kujua ukweli wa maisha nenda makaburini! Huko ni uozo na mifupa! Wamekuwa chakula cha sisimizi na siafu. Ee Mwenyezi Mungu, mtu ni nini! Ingawa alisifika sana! Ingawa alijiinua sana! Alijipenda sana! Alikuwa na watumishi wengi! Na kila alipopita alisujudiwa kutokana na fedha zake! Cheo chake! Haiba yake! Leo hii yuko makaburini! Kimya kabisa! Amegeuka kuwa chakula cha mchwa! Ama kweli binadamu hatadumu katika fahari yake! (Zab 49).
Heri yenu ninyi watakatifu! Mlifahamu namna ya kutokuandama na mwili na kama mlifanya chochote mliienzi roho yenu. Mliishi mkitoa kipau mbele kwa Mungu ambaye kwa maisha yenu ya duniani mlimpenda kwa kuwa ndivyo ilivyowapasa. Mlifunga ili kuunidhamisha mwili ili usiwe kikwazo cha kumtumikia Mungu.
Kwa uaminifu wenu, sasa ingawa mlikufa kuhusu mwili mifupa yenu sasa inaheshimiwa kama masalia matakatifu.mlielewa ukuu wa mwanadamu na kwa sababu hiyo mliuzingatia ukweli wa maisha na sasa mnafurahia heri ya mbingu, mkisubiri siku za mwisho ambapo miili yenu itashiriki katika utukufu mtakaopewa kwa kushiriki maisha ya kristo katika ulimwengu huu. Upendo wa kweli kuhusu mwili katika maisha haya ni pamoja na kuunidhamisha, kufunga na kujikatalia hata starehe halali, ili siku moja pamoja na roho yako mpokee tuzo ya heri ya milele.
Sala
Ee Mungu wangu, mimi ni sawa na ule mti ambao umestahili kusikia maneno yale ya hukumu: “Ukate. Kwa nini unaendelea kuinyonya ardhi?” Ndiyo Bwana mpaka sasa sijaweza kuzaa matunda yenye heri mbali na miiba ya dhambi zangu.
Hata hivyo Bwana Mungu, si mpango wako niishi kwa kukata tamaa. Umesema kwa wote wanaokutafuta watakupata: “Nitafuteni maadamu ninapatikana.” Mt 7:7. Umesema pia” “Ninyi mkiomba lolote kwa jina langu, hilo nitalifanya, ili Baba atukuzwe ndani ya mwana.” Yn 14:14.
Ee Yesu mwema na mpenzi wangu, nikijiaminisha katika ahadi hizi zako, na katika jina lako na kwa mastahili yako, ninaomba neema na upendo wako. Unijalie ili kwamba neema zako za kimungu na upendo wako vitawale moyoni mwangu ambako hapo zamani dhambi ilitamalaki.
Bikira Maria mama yangu na mwombezi wangu, usikie kilio changu na uniombee kwa Yesu. Amina.

Post a Comment

 
Top